Hadithi za kale zenye mafundisho za Esopo zilizoandikwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Zimetafsiriwa kwa Kiswahili na Issa S. Kanguni, chini ya shirika lisilo la kiserikali la Tanzania Inventors and Techno-Thinkers Consortium (TITC). Tel; +255757242960

Tafuta katika Blogu Hii

Pages

Jumatatu, 23 Desemba 2013

KISA CHA SIMBA NA PAPA

Siku moja Simba alikuwa akirandaranda ufukweni mwa bahari, akamwona Papa akichomoza kichwa chake juu ya uso wa bahari katikati ya mawimbi. Alizama na kuibuka tena… akazama na kuibuka tena… Simba alivutiwa naye na kumwona kuwa anafaa kuwa rafiki kwani ni mkubwa na mwenye nguvu kama yeye.

Alimwita karibu naye akasogea.
Baada ya kusalimiana Simba akamshauri mwenzake kuwa ipo haja ya kufanya makubaliano ya ushirikiano na urafiki baina yao, akimchagiza kuwa kati ya wanyama wote wa mwituni, wao Simba na Papa ndiyo wapaswao kuwa maswahiba haswa. Kwani mmoja wao ni mfalme wa wanyama wote wa nchi kavu ilhali mwingine ni mtawala wa viumbe wote wa baharini.

Papa alilipokea wazo hilo la Simba kwa mikono miwili. Wakakubaliana.
Punde akatokea Mbogo, na Simba, kwa kuwa alikuwa na njaa alimtamani na kuanza kupambana naye. Simba alipoona analemewa aliamwita rafikiye Papa aje nchi kavu kumsaidia.
Papa, ingawa alikuwa na nia ya dhati ya kumsaidia, hakuweza kufanya hivyo kwani hakuwa na namna yoyote ya kuweza kutoka majini.

Simba akamshutumu na kumdhihaki Papa kuwa ni muasi na asiye mwaminifu.
Papa akamjibu; “Hapana rafiki yangu, wala sistahili mzigo huo wa lawama toka kwako, yakupasa umlaumu muumba, ambaye, pamoja na kunipa ukuu na utawala majini, ameninyima kabisa uwezo wa kuishi juu ya nchi kavu.”
Share:

0 maoni:

Chapisha Maoni

Live Traffic Feed

Blogroll

BTemplates.com

Inaendeshwa na Blogger.

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Popular Posts

Kumbukumbu la Blogu