Hadithi za kale zenye mafundisho za Esopo zilizoandikwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Zimetafsiriwa kwa Kiswahili na Issa S. Kanguni, chini ya shirika lisilo la kiserikali la Tanzania Inventors and Techno-Thinkers Consortium (TITC). Tel; +255757242960

Tafuta katika Blogu Hii

Pages

Jumatatu, 16 Juni 2014

KISA CHA NYANI WACHEZA SHOO

Mwanamfalme aliagiza Nyani kadhaa wapewe mafunzo maalum ya kucheza shoo. Kwa  vile kwa asili Nyani ni waigaji wazuri sana wa matendo ya binadamu, walionyesha kuwa wanafunzi bora wenye kushika mafuzo haraka, na walipovishwa nguo na vinyago kichwani, walicheza vizuri sana hadi kulingana au kwazidi wacheza shoo binadamu. 

Kwenye matamasha maonyesho yao mara nyingi yalishangiliwa kwa vifijo na nderemo, hadi siku moja jamaa fulani mcheza shoo mwenye wivu, aliyepania kuwafanyia hila, alitoa mfukoni mwake karanga za maganda na kuzirusha jukwaani. 
Basi ikawa wale Nyani, baada ya kuona karanga wakasahau kazi yao ya kucheza na wakawa (na kweli walikuwa) Nyani badala ya Wachezashoo
Walivua vinyago vyao na kuchanachana nguo walizovikwa, wakagombania karanga. Hivyo onyesho hilo likaishia hapo huku hadhira ikicheka na kudhihaki.
***
Share:

Kisa cha Wavulana na Vyura


Watoto wavulana, wakiwa wanacheza kandokando ya bwawa, waliona Vyura kwenye maji wakaanza kuwarushia mawe huku wakifurahia mchezo wa kulenga shabaha. 
Waliwaua vyura kadhaa, hadi Chura mmoja jasiri, alipotokeza kichwa chake nje ya maji, na kuwaambia kwa uchungu: 
"Acheni, acheni, enyi vijana: huu ambao ni mchezo kwenu, kwetu sisi ni kifo."
Share:

Kisa cha Mbwa na Mbweha

Mbwa, katika pitapita zao waliikuta ngozi ya Simba, wakaanza kuing'ata na kuirarua vipande vipande kwa meno yao. 

Mbweha aliwaona, akawaambia, 
"Laiti kama Simba huyo angekuwa hai, basi bila shaka mngetambua ya kuwa makucha yake yana nguvu kuliko hata meno yenu."
Share:

Jumamosi, 31 Mei 2014

KISA CHA NYIGU NA NYOKA

Nyigu alitua kwenye kichwa cha Nyoka na kuanza kumng’ata mfululizo, akimjeruhi vibaya kwa lengo la kutaka kumwua. 
Nyoka, akiwa katika maumivu makali asijue namna ya kujiokoa na adui yake huyo, mara akaona mkokoteni uliojazwa magogo ya miti ukipita. 

Basi kwa makusudi akaamua kwenda njiani na kuweka kichwa chake chini ya gurudumu, akasema, 
“Angalau, mimi na adui yangu tuangamie sote pamoja.”
***

1. Hadithi hii inatufundisha nini?
2. Taja methali au nahau ya kiswahili yenye maana sawa na maudhui ya hadithi hii.
Share:

KISA CHA MITUNGI MIWILI

Mitungi miwili iliachwa kwenye ukingo wa mto, mmoja wa chuma, na mwingine wa udongo. 
Baada ya mvua kubwa kunyesha mbali mto utokako ndipo maji ya mto yalipoongezeka na hatimaye mitungi yote ilisombwa ikaelea kufuata mkondo. 

Basi ule mtungi wa udongo ukawa unafanya jitihada kwelikweli kujiweka mbali na ule wa chuma. Kuona vile, Mtungi wa chuma ukatabasamu na kuuambia ule wa udongo: 
“Usihofu rafiki yangu, mi sikugongi.”


“Sawa, lakini inawezekana nikagusana nawe,” ukasema mtungi wa udongo, “iwapo nitakukaribia; kwani haijalishi wewe ukinigonga, au mimi nikakugonga, nitadhurika tu.”
***
Share:

Ijumaa, 30 Mei 2014

KISA CHA MAADUI WAWILI

Jamaa wawili, ambao walikuwa ni maadui wa kufa na kupona, walijikuta wakisafiri katika merikebu moja. Wakiwa wamepania kukaa mbalimbali kadri iwezekanavyo, mmoja alienda kukaa nyuma kabisa na  mwingine mbele kabisa kwenye ncha ya mwisho ya merikebu. 

Mara kukapiga dhoruba kali na mawimbi yakaanza kukipeleka chombo mrama, na kilipokuwa kwenye hatari ya kuzama, yule jamaa aliyekaa nyuma akamuuliza nahodha ni upande upi wa merikebu ile ungelianza kuzama kabla ya  mwingine. 
Alipomjibu kwamba anaamini ni upande wa mbele utakaozama kwanza, yule jamaa akasema, 
“Kifo hiki hakitokuwa na mateso kwangu, endapo tu nitafanikiwa kumwona yule rafiki yangu pale akitapatapa na kufa kabla yangu.”
***
Share:

KISA CHA PANYA WA MJINI NA PANYA PORI

Panya Pori alimwalika panya wa mjini, ambaye ni rafiki yake kipenzi, amtembelee kwake aje ajionee maisha ya porini. Wakiwa kwenye uwanda wazi wa mashamba, wakila mabaki ya nafaka na mizizi ya miti iliyong’oka, Panya wa Mjini alimwambia rafiki yake, 
 “Huku shamba rafiki yangu unaishi maisha ya wadudu, yaani kama mchwa ama sisimizi, wakati mimi kule nyumbani kwangu ni neema tupu ya vyakula kedekede.  Yaani nimezungukwa na kila aina ya raha na anasa, na iwapo utakubali kufuatana nami nyumbani, kama ninavyoamini utakubali, nawe utapata kufaidi sehemu ya mapochopocho yangu.” 

Kwa maneno yale, Panya Pori akashawishika kiurahisi, na akakubali kuandamana na rafiki yake katika safari ya kurudi mjini. Walipofika, Panya wa Mjini akamtengea rafikiye mlo wa mkate, shayiri, maharagwe, matini yaliyokaushwa, asali, zabibu kavu, na, mwishowe, alimletea kipande kinono cha jibini toka kapuni. Panya Pori, akiwa na furaha isiyo kifani kwa kupata chakula kizuri na kingi kama kile, alishukuru kwa unyenyekevu na kuyalaani maisha yake magumu kule shamba. 

Basi wakiwa ndo wanataka kuanza kula, bwana mmoja akafungua mlango, na wote wawili wakatimka mbio kadri ya uwezo wao na kuingia kwenye kijishimo chembamba kilichowatosha kwa kujibana. Baadaye wakatoka, na kwa mara nyingine kabla hata hawajaanza kula, mtu mwingine akafungua mlango na kuingia kuchukua kitu fulani kabatini, ambapo wale panya wawili, wakiwa na hofu zaidi ya mara ya kwanza, walikimbia na kwenda kujificha tena. 

Mwishowe yule Panya Pori, huku akitweta na akiwa ameshikwa na njaa kwelikweli, akamwambia rafiki yake: 
“Japokuwa umeniandalia mlo maridhawa, sina budi kuondoka na kukuachia uufaidi mwenyewe. Chakula chako kimezungukwa na hatari nyingi mno, siwezi kukifurahia hata kidogo.  Kwangu mimi ni heri maisha ya  kuokoteza nafaka na kuguguna mizizi porini, ambako ninaishi kwa usalama, bila hofu yoyote.”
Akaenda zake.
***
Share:

KISA CHA MBWA WAWILI

Kulitokea bwana mmoja ambaye alifuga mbwa wawili: 
Mbwa mwindaji, ambaye alimfundisha kumsaidia katika kazi zake za uwindaji, na Mbwa mlinzi, aliyemfundisha kulinda nyumba. 

Kila aliporejea nyumbani kutoka mawindoni, alikuwa akimpa yule Mbwa wa nyumbani minofu mikubwa mikubwa ale. Mbwa mwindaji hakupendezwa na jambo lile na alishindwa kuvumilia, alimfuata mwenzie, akamwambia, 

“Ni mateso makubwa kufanya kazi ngumu kama nifanyayo mimi, ilhali wewe, ambaye husaidii lolote katika kuwinda, unajibarizi na kufaidi matunda ya jasho langu.” 

Mbwa wa nyumbani akamjibu, 
“Rafiki yangu, usinilaumu mimi bali umlaumu bwana wetu, ambaye hajanifundisha mimi kufanya kazi bali kuishi kwa kutegemea matunda ya kazi za wengine.”
***
Share:

Alhamisi, 22 Mei 2014

Kisa cha Bwana Mzalendo mwenye Kipawa

Baada ya kufanikiwa kupewa nafasi ya kusikilizwa na mfalme na baraza lake la washauri, Mzalendo mwenye kipaji alitoa karatasi mfukoni mwake, akasema: 
Share:

Jumapili, 18 Mei 2014

KISA CHA TAI, PAKA NA NGURUWE PORI

Kulitokea Tai mmoja ambaye alijenga kiota chake juu ya mti mkubwa; Paka naye, baada ya kuona kuna shimo linalomfaa, alihamia na kuanza kuishi katikati ya shina la mti ule ule; na Nguruwe pia, akiwa na vitoto vyake, akaweka makazi kwenye shimo lililopo wazi chini ya mti ule. 

Basi ikawa Paka, kwa tabia yake mbaya, akaanza kutengeneza hila ili kuvuruga kusanyiko lile la kudra la familia tatu tofauti katika mti mmoja. Ili kutekeleza njama yake, alianza kwa kupanda juu kwenye kiota cha Tai, akamwambia, 
"Ndugu yangu, angamizo linakaribia kushuka juu yako, na mimi pia, kwa bahati mbaya. Jirani yetu Nguruwe-pori, ambaye unamwona kila siku akichimbua chimbua ardhi kwa mdomo wake, anataka kuung'oa mti huu, ili utakapoanguka akamate familia yako na yangu kwa ajili ya chakula kwa watoto wake." 

Baada ya kufanikiwa kumwogofya Tai kiasi kile, Paka alishuka chini kabisa na kwenda kwenye shimo la Nguruwe-pori, akamwambia, "Ndugu yangu, maisha ya watoto wako yapo hatarini; kwani punde tu utakapothubutu kutoka kwenda kutafuta chakula, Tai amejiandaa kushambulia mmoja wa watoto wako, kwa ajili ya chakula cha familia yake." 
Alipofanikiwa kumjaza hofu Nguruwe-pori, Paka akaenda zake kwake na kujifanya kana kwamba naye anajificha kwa woga kwenye shimo lake. Ilipofika nyakati za usiku kila siku alinyata na kutoka kinyemela kwenda kutafuta chakula kwa ajili yake na wanawe, huku akijifanya kuogopa na kuwalinda wanawe mchana kutwa.

Wakati huo, Tai,  akiwa ana hofu kuu dhidi ya Nguruwe-pori, alikaa kwenye kiota chake kutwa kucha, ilhali Nguruwe pori naye, akiwa na hofu kuu dhidi ya Tai, hakuthubutu kutoka kwenye shimo lake. 
Kwa hali hiyo, wote pamoja na familia zao, waliangamia kwa njaa, na kumwacha Paka na wanawe wakijivinjari kwa nafasi.
***
Share:

KISA CHA MARAFIKI WAWILI NA DUBU

Marafiki wawili walikuwa wakisafiri pamoja kupitia vichakani, mara akatokea dubu mkubwa na kuanza kuwakimbiza.
Katika harakati za kutaka kujiokoa walikimbia na ikawa mmoja kati yao alikuwa mbele na mwingine nyuma yake. 

Basi yule wa mbele iliwahi kulishika tawi la mti na kujificha peke yeke kwenye majani. Mwenzake, kwa kuona amechelewa na hana namna, alijitupa chini na kulala kifudifudi, huku akijilegeza kama mfu. Dubu alipomfikia, aliweka pua yake sikioni kwa yule bwana, akanusa na kunusa. 

Mwishowe, Dubu akaguna kwa nguvu huku akijitikisa kichwa na kuenenda zake, kwani Dubu huwa hawali mizoga. 

Ndipo yule bwana aliyejificha peke yake kwenye mti akaja kumfuata rafiki yake, na, huku akicheka, akasema "Kakunong'oneza nini yule bwana mkubwa?" 
"Ameniambia kwamba," alijibu yule bwana, "Kamwe usimwamini rafiki anayekutelekeza wakati wa shida."
***
Share:

Jumamosi, 17 Mei 2014

KISA CHA BAHILI NA DHAHABU ZAKE

Bwana mmoja bahili aliuza vitu vyake vyote alivyonavyo na kununua sarafu za dhahabu, ambazo alichimba shimo na kuzifukia chini kando ya ukuta wa zamani na kuwa anakwenda kuziangalia kila siku. Mmoja wa wafanyakazi wake aligundua safari zake za mara kwa mara kwenda eneo lile na akaanza kumchunguza zaidi. 

Muda mfupi tu baadaye aling'amua siri ya ile hazina iliyofichwa, na alipochimbua na kukuta rundo la dhahabu, akaziiba. Yule bwana bahili, alipofika siku iliyofuata, alikuta shimo tupu na akaanza kulia na kuvuta nywele zake hata kuzinyofoa kwa hasira na majonzi. Jirani yake, baada ya kumwona akiwa katika hali ile ya huzuni kupita kiasi, na alipogundua sababu ya huzuni ile, alimwambia 
"Ndugu, hakuna haja ya kuhuzunika kiasi hicho; bali nenda na uchukue jiwe, liweke humo shimoni na ufunike, kishakila siku kuangalia na jifanye kana kwamba dhahabu zako bado zimo humo. Itakufaa kwa hali ile ile; kwani hata kabla ya kuibiwa haukuwa nayo dhahabu, kwa kuwa uliifukia tu na hukuitumia kwa namna yoyote ile."
***
Share:

KISA CHA MBWA NA MBWA MWITU

Mbwa-mwitu mmoja dhaifu alikuwa akikaribia kufa kwa njaa na mara kwa bahati akakutana na mbwa wa nyumbani ambaye alikuwa akipita. 
"Ah, binamu," alisema mbwa "nilijua tu yatakukuta haya; kwamba maisha yako ya kutangatanga na yasiyo na uhakika ipo siku yatakuangamiza. Kwanini usifanye kazi maalum na ya uhakika kama nifanyavyo mimi, ili upate chakula kila mara kama nipatavyo  mimi?" 
"Nakubaliana na wewe kabisa ndugu yangu," alijibu Mbwa-mwitu, "endapo tu nikipata nafasi." 
"Nafasi sio tatizo, mi ntakufanyia mpango," alisema Mbwa; "twende nami nyumbani kwa bwana wangu na nitamwomba akuajiri tufanye kazi pamoja nami." 

Basi Mbwa-mwitu na Mbwa wakaongozana kuelekea mjini. Wakiwa bado njiani, wanakaribia kufika Mbwa-mwitu akagundua kwamba nywele kwenye sehemu fulani ya shingoni ya Mbwa zimenyonyoka na kubaki chache, hivyo akamuuliza Mbwa kulikoni. 
"Oh, wala si kitu," Mbwa alijibu. "Hii ni sehemu ambayo mkanda wa nyororo hufungwa nyakati za usiku ili kunifanya nibaki sehemu moja; unauma na kukera kidogo, ila baada ya muda unazoea." 

"Ha ndiyo hivyo?" alisema mbwa mwitu. "Basi kwaheri ndugu yangu, Bwana Mbwa."
***
Share:

KISA CHA MBWA NA SUNGURA

Mbwa mwindaji alimvumbua Sungura kwenye mafukutu juu ya kilima na kuanza kumkimbiza kwa kitambo, wakati fulani alimkaribia na kung'ata kwa nguvu kwa meno yake makali kana kwamba ataka kumuua, na mara nyingine alimkumbatia kana kwamba anacheza na mbwa mwenzake.

 Yule Sungura akamwambia, "natamani ungekuwa mkweli kwangu, na kuonyesha dhamira yako halisi. Kama we ni rafiki, kwa nini umening'ata kiasi hiki? na kama we ni adui, kwa nini basi unacheza nami?"
***
Share:

KISA CHA MZEE KIPARA NA MBUNG'O

Mbung'o alitua kichwani kwa Mzee mmoja na kumng'ata kwenye sehemu yenye kipara, ambapo yule Mzee kwa kutaka kumwangamiza Mbung'o alijipiga kofi pwaaa! 

Yule mbung'o alifanikiwa kukwepa na aliondoka akisema kwa dhihaka, 
"Ulipanga kulipiza kisasa, hata kwa kuua, maumivu madogo tu ya kung'atwa na mdudu kama mimi, ona sasa ulivyojitenda na kujiongezea maumivu juu ya maumivu?"

 Mzee kipara akamjibu, 
"Ni rahisi kwangu kujisamehe maumivu ninayojipa mwenyewe, kwani najua hakukuwa na nia ya kujiumiza. Lakini wewe, mdudu baradhuli mwenye tabia ya kunyonya damu za watu, natamani ningelifanikiwa kukuua hata kama ningalipata maumivu makubwa zaidi ya haya niliyopata sasa."
***

Share:

KISA CHA MAMA NA MTETEA

Hapo zamani za kale kulikuwako mama mmoja ambaye alikuwa na kuku wake mtetea aliyetaga yai moja kila siku.

 Kila wakati yule mama alifikiri na kujiuliza atawezaje kupata mayai mawili kwa siku badala ya moja, na mwishowe, ili kutimiza azma yake, akaamua kuanza kumlisha yule kuku mara mbili ya shayiri za chakula alichokuwa akimpa kwa siku.

Basi kuanzia siku hiyo yule kuku alinenepa
sana na kuwa mtepetevu, na hakutaga tena.
***

Share:

KISA CHA MBWEHA ALIYEKATWA MKIA

Hapo zamaini za kale, kulitokea Mbweha mmoja mjanja. Siku moja kwenye pitapita zake kwa bahati mbaya alinaswa mtegoni, na katika kuhangaika alifanikiwa kujinasua, ila alikatika mkia ukabakia kipisi kifupi tu.

Siku za mwanzo mwanzo aliona aibu kujionyesha ulemavu wake wa kutokuwa na mkia kwa mbweha wenzake. Baadaye akaamua kujibaraguza na kufanya kana kwamba kukosa mkia si kitu, akawaalika Mbweha wote kwenye mkutano mkuu, ili wajadili pendekezo alilo nalo moyoni.

Walipokusanyika, Mbweha alitangaza pendekezo lake, kwamba eti mbweha wote ni vyema wakakata mikia yao na kubaki na vipisi kama yeye.  Akasema kwamba mkia ni mzigo wanapokuwa wanafukuzwa na maadui zao, mbwa; na pia unasumbua wanapohitaji kuketi kitako wazungumze mambo kirafiki na wenzi wao. Akapaza sauti na kudai kuwa haoni faida yoyote ya wao kuendelea kubeba zigo la mkia usio na tija yoyote.

“Hiyo ni sawa kabisa,” akajibu mbweha mmoja mzee; “ila sidhani kama ungelitoa pendekezo la kukata mikia ambayo ni kifaa chetu muhimu, laiti kama wewe mwenyewe usingalipatwa janga la kupoteza mkia wako.”
***
Share:

Jumatano, 7 Mei 2014

KISA CHA MBWEHA, MBWA MWITU NA NYANI

Mbwa mwitu alimshutumu  vikali Mbweha kwa kumwibia, ila Mbweha alikana katukatu kwamba hakutenda kosa hilo. Baada ya kuzozana kwa muda, wakampelekea Nyani shauri hilo ili atoe hukumu na kumaliza mgogoro baina yao. 

Basi baada ya kila mmoja wao kupewa nafasi ya kujieleza kwa kina, Nyani akatangaza hukumu ifuatayo: 
"Siamini katu kwamba wewe, Mbwa mwitu, umepotelewa na hicho unachodai kuibiwa; na ninaamini kabisa kwamba wewe, Mbweha, umeiba hicho unachokataa katakata kuwa hujaiba."
***

Hadithi hii inatufundisha nini? Jibu ujishindie.
Share:

KISA CHA WASAFIRI WAWILI NA SHOKA

Jamaa wawili walikuwa wakisafiri pamoja. Wakiwa njiani mmoja wao aliokota shoka zuri lililokuwa limelazwa kando ya njia, akalichukua na kusema, 

"Nimeokota shoka." 
"Hapana rafiki yangu," mwenzake alimjibu, "usiseme 'Nimeokota' bali 'Tumeokota' shoka." 

Basi kabla hata hawajafika mbali wakamwona mwenye shoka lake akiwafuata kwa hasira, ndipo yule aliyeliokota shoka akasema, "Duh! tumekwisha." 

"La hasha," alijibu yule mwenzake, "endelea na ile kauli yako ya awali, rafiki yangu; kile ulichoona sahihi wakati ule, kione kuwa sahihi hata sasa. Sema 'Nimekwisha', sio 'Tumekwisha'."
***
Share:

Jumatano, 30 Aprili 2014

MIFUKO YA DHAMBI

Kwa mujibu wa masimulio ya ngano za kale za mababu zetu, eti inasemekana kwamba kila binadamu hapa duniani amezaliwa na mifuko miwili ikining'inia shingoni mwake. 

Fuko kubwa la mbele linajazwa mapungufu na madhambi ya majirani zake, na fuko kubwa linaloning'inia nyuma linajazwa mapungufu na madhambi yake mwenyewe.

 Ndiyo maana watu ni wepesi kuona na kulaumu makosa ya wenzao, huku mara nyingi wakishindwa kutambua mapungufu yao wenyewe.
***
Share:

KISA CHA MWINDAJI NA MVUVI

Mwindaji, akiwa na mbwa wake anarejea kutoka mawindoni, kwa bahati alikutana na Mvuvi ambaye naye alikuwa anarejea nyumbani toka ziwani na kapu lake lililojaa samaki. 

Basi ikawa yule Mwindaji akatamani sana wale samaki kwenye kapu la Mvuvi, ilhali yule Mvuvi naye alitamani sana kitoweo kilichopo kwenye mkoba wa yule Mwindaji.

Kwa hiyo mara moja wakakubaliana kubadilishana mawindo yao ya siku kwa Mvuvi kuchukua mkoba wa Mwindaji na Mwindaji kuchukua fuko la samaki. Kila mmoja alifurahia sana makubaliano yale kiasi cha kwamba waliendelea kufanya vile siku hadi siku.
 
Mwishowe jirani yao mmoja akawaambia, "Enyi wandugu, iwapo mtaendelea kwa mwenendo huu, muda si mrefu mtaharibu raha ya kubadilishana kwa kuwa mnabadilishana kila siku, na hatimaye kila mmoja wenu atapenda abaki na chake."
***
Share:

KISA CHA MPIGA-TARUMBETA VITANI

Hapo zamani za kale, kulikuwapo bwana mmoja mpiga tarumbeta ambaye alikuwa jasiri akiwaongoza askari  vitani. 

Basi siku moja huku vita ikiwa imepamba moto, alisogea kuwakaribia maadui kupita kiasi, matokeo yake akakamatwa. Wakati wakijiandaa kumnyonga, akaanza kulia na kubembeleza asiuawe na badala yake aachiwe huru, "Tafadhalini niacheni, msiniue nihurumieni kwa kuwa mimi sina hatia" akasema "mimi si mpiganaji, sijaua mtu yeyote, na sina hata silaha. Mi napiga tu tarumbeta hili, na kwa kweli sidhani kama hiyo inamuumiza yeyote kati yenu. Sioni sababu ya nyie kunidhuru!"

"Ingwa haupambani mwenyewe" wakamjibu "lakini unapopiga tarumbeta lako unawahimiza na kuwaongoza watu wako kupambana nasi. Na hiyo ni sababu tosha kukuadhibu."
Share:

Jumapili, 27 Aprili 2014

KISA CHA WEZI NA JOGOO

Vibaka walivunja nyumba ili wakaibe na walipoingia ndani hawakukuta kitu chochote isipokuwa jogoo. Wakamkamata jogoo yule na kuondoka naye haraka. 

Walipofika kwao walijiandaa kumchinja jogoo watengeneze kitoweo, ambapo jogoo alianza kujitetea asiuawe: “Tafadhalini msinichinje; ni vyema mkanifuga kwani ninasaidia sana watu. Ninawaamsha watu usiku ili wawahi makazini kwao.”

 “Hiyo ndiyo sababu mojawapo inayotufanya lazima tukuchinje” wakamjibu “kwani kila unapowaamsha majirani zako, unatuharibia sisi na unakatisha muda wetu wa kazi.”
***


Share:

KISA CHA KIBAKA NA MAMAYE

Hapo zamani za kale kulikuwepo mvulana mmoja aliyeishi na mama yake. Siku moja, akiwa shuleni kijana aliiba kitabu cha mwanafunzi mwenzake na kurudi nacho nyumbani akamwonyesha mama yake. Yule mama, sio tu hakumchapa wala kumgombeza, bali alimpongeza. 

Kijana akakua kuelekea utu uzima, huku akiendelea na tabia yake ya wizi wa vitu vikubwa zaidi. 

Wanasema za mwizi arobaini. Mwishowe ilitokea siku akakamatwa akijaribu kutaka kuiba, na akiwa amefungwa mikono yake kwa nyuma na wananchi wenye hasira, akapelekwa kwenye uwanja maalum ambapo wahalifu hupewa adhabu ya kunyongwa hadharani. 

Mama yake naye akafuata msafara akilia na kujipigapiga kwa huzuni na uchungu wa mwanaye, ambapo yule kijana kuona vile akasema, “Naomba kuongea na mama yangu nimnong'oneze jambo tafadhali.” Mama yake akamsogelea kumsikiliza. 
Basi yule kijana alimng'ata sikio kwa nguvu nusura anyofoe kipande.

Mama yake akamfokea na kumtolea maneno ya kumlaani kwamba ni mtoto mbaya, naye akajibu “Ah! Laiti ungalinichapa na kunikemea siku ya kwanza nilipoiba na kukuletea kile kitabu, yasingenifika haya, na wala nisingalikufa kifo cha aibu kama hiki.”

***
Share:

Jumatano, 23 Aprili 2014

NIPE RISITI - La Sivyo...




Onyo; Hadithi hii ni ya kubuni (fiction) na haina uhusiano na tukio lolote lililowahi kutokea. Majina ya wahusika na tabia zao hazina uhusiano na mtu yeyote halisi hivyo ikitokea aina yoyote ya kufanana ni bahati mbaya tu. 

Mtunzi; Issa S. Kanguni
0757242960 /  0655242960
ibot.isk@gmail.com

Haki zote zimehifadhiwa.




Chapter One

          Sauti na kikiri kakara toka chumba cha pili zilimshtua kutoka usingizini. Alitupa shuka kando, akajiviringisha upande na kujiinua kiwiliwili. Akafikicha macho kwa mkono wa kushoto na kushusha miguu chini kabla ya kunyanyuka na kusimama wima huku vifundo vya miguu vikaalika na mapaja yake laini kusisimka. Alipapasa kiberiti awashe kibatari akasita. Akiwa mtupu vilevile bila kujisitiri alitembea kwa kunyata hadi mlangoni kuhakiki kama kweli jana kabla ya kulala aliufunga kwa komeo. Aliporidhika akatembea tena kwa kunyata hadi kwenye kidirisha kidogo upande wa pili wa chumba chake. Akachungulia nje. Bado giza... hakujapambazuka. Nyimbo hafifu za ndege zilizosikika toka mabondeni mbali zilimpa hakika kwamba pambazuko lilikuwa limekaribia. Kiupepo cha ubaridi kilipuliza kuashiria mwanzo wa msimu wa kipupwe.  
          Nia yake ilikuwa ni kuondoka kukiwa bado giza na alijua ana dakika chache tu zakujiandaa na kutoka, vinginevyo mpango mzima ungelivurugika.
          Maandalizi ya kila kitu alishayafanya tangu usiku kabla ya kulala. Giza lilijaribu kumzuia asione, halikufanikiwa.
Alisogea kitandani akafunua godoro mchagoni na kulishikilia kwa mkono wa kushoto huku mkono wa kuume ukipapasa papasa na hatimaye kutoa kitita cha nguo zilizokunjwa vizuri. Harakaharaka akashusha godoro na kuanza kuvaa. Alianza boxer mpya nyeupe yenye urembo wa kung’aa ng’aa na picha ya mkuki moyoni, halafu suruali ya jinsi nyeusi ya kubana, akafunga mkanda. Kisha akavaa sidiria tatu, ya kwanza nzito nyeupe, ya pili nyeupe tena na ya tatu nyeusi. Zilimkaa vyema.  Halafu akaikunjua na kuivaa blauzi ya rangi ya kijivu yenye madoadoa ya pinki na mikunjo shingoni, na baada ya hapo akavaa wigi lenye nywele ndefu kichwani. Alipomaliza, alikuwa na mwonekano wa msichana wa miaka mitana zaidi ya umri wake. Just how she wanted!
“Leo ndio leo…” alijisemea kimyakimya “ama zao ama zangu. Kama wanajifanya wao ndo wanajua mapenzi sasa leo ndo mwisho wao.”
Aliinama akafungua kishubaka cha kitanda na kutoa vifaa vyake vya kazi, kibunda cha pilipili ya unga, nyembe tatu mpya, na kifaa maalum alichokibuni na kukiunda mwenyewe na kukiita kwa kifupi FZ (anatamka efzii), akaviweka kwenye mkoba mweusi pamoja na miwani ya giza, mtandio na kamba ya nailon.
          Alivaa raba, akafunga gidamu. Alisimama akajinyoosha na kujiweka sawa. Aliuweka mkoba begani na kutembea kwa uangalifu hadi mlangoni, akanyoosha mkono ili afungue, mara akasikia mlango wa chumba cha pili unafunguliwa. Akasubiri.
“Hapa leo huendi… kama hutaki twende wote huendi…” sauti ya mwanamke ilisikika ikisema kwa  kulalamika.
“Haya… mdomo si mali yako. Lalama weeee, mwisho wa siku mi siwezi kukatisha safari yangu.” Mwanaume alijibu taratibu kwa dharau.
“Twende sote… kwani kuna tatizo gani tukienda sote?” alihoji mwanamke.
“Kwani n’kienda peke yangu kuna tatizo gani?”
“Kuna tatizo gani!... yaani unauliza kuna tatizo gani? Kwani we hujui? …huendi. La kama uk’enda peke yako basi usichukue pesa zote, chukua nusu.”
“Ili?”
“Ukienda na pesa zote ndo haurudi tena wewe… hadi ziishe..”
“Unaota wewe…” akamsonya “… unajifanya unataka kunilinda mimi utaweza wapi… nipishe huko. Unasahau ni nani kamwoa mwenzie humu ee… sasa kwa taarifa yako… ipo’ivi… kadri unavyozidi kujifanya unanipangia masharti ndo kwanza unazidi kunichefua. Kwa mfano, nilipanga kuacha kiasi cha pesa sasa…” ilisikika sauti ya zipu ikifunguliwa kwa nguvu “…nachukua zote. Funga domo lako. Na umesema sitorudi hadi ziishe… well… omba mungu…”
“Lakini kwa nini mume wangu unanifanyia hivi!... mbona unapokuwa huna pesa tunakaa vizuri… sasa…”
“Aaagh… haukomi tu na mahubiri yako we mwanamke… sasa leo n’takuonyesha… na tena ndo kwanza unasababisha n’ondoke kabla ya mawio. N’mekuchoka… mwanamke gani wewe… sura mbaya na gubu haviendi… afu tena unasahau sheria inaniruhusu kuwa na wangapi.”
“Lakini kumbuka tulikotoka mume wangu.”
“Tulikotoka?... ipo’ivi… sahau tulikotoka. Ndo’ubovu wa uchumba wa kushinikizwa na wazazi… we kwa akili yako unadhani kosa kushinikizwa ni n’ngekuoa wewe na matege kama hayo!? No. na hata kama n’ngekuoa ingelikuwa ni kwa maamuzi yangu mwenyewe si kwa shuruti ya wazazi kisa etu una tabia njema… haya sasa tabia njema i wapi leo...”
Mwanamke alijaribu kusema jambo akashindwa. Akaanza kulia kwa uchungu. Ni dhahiri haikuwa mara yake ya kwanza kusemwa na kutendwa vibaya katika ndoa yake, ila kudharauliwa kulimuuma sana. Na mume wake hakuwa mwepesi wa kuinua mkono kupiga, bali ulimi. Mara zote alilenga kujeruhi moyo, si mwili. Alisikika akijitupa chini na kuanza kulia… kilio cha yaliyopita, yaliyopo, na yajayo.
 Mlango ukabamizwa, sauti ikakoma. Nyayo zilisikika zikipita kwenye ususu kwa haraka kisha mlango wa kutokea nje ukafunguliwa, halafu baadaye ule wa maliwatoni.
Alijua kinachoendelea nje. Alijua anachopaswa kufanya.
          Bila kupoteza muda, hasira zake zikiwa zimeongezeka maradufu, alifungua mlango akatoka na kuufunga nyuma yake. Alipiga hatua ndefu ndefu na kufika kwenye mlango wa nje ambao uliachwa wazi akachungulia nje kwa tahadhari kisha akainama na kutoka taratibu. Sekunde chache baadaye alijikuta uchochoroni nje ya nyumba kukiwa bado na giza. Hasira na chuki dhidi ya baba yake, na huruma na upendo kwa mama yake vilisaidia kumwondoa woga ingawa ilikuwa ndo mara yake ya kwanza kutoka nyumbani kwao katika muda na staili kama ile. Mawingu yalianza kujongea kugubika anga na kufanya giza liwe totoro. Akatafuta sehemu nzuri ya kujibanza kando ya barabara chini ya mti. Sauti kali ya bundi ilisikika ikitokea kwenye moja kati ya miti mitatu mikubwa jirani na pale alipojificha. Hakujali.

          “Leo ndo leo… ama zao ama zangu.” Alijisemea tena kwa sauti yenye hisia kali ya kisasi na kupania. Alifungua pochi kutoa mtandio huku akiangaza kila upande, akajitanda na kuketi kwenye kigingi. Akasubiri…

Itaendelea....


Share:

Jumapili, 20 Aprili 2014

KISA CHA NJIWA MWENYE KIU





Njiwa, akiwa amezidiwa na kiu kupita kiasi, aliona picha ya mtungi wa maji iliyochorwa kwenye bango. 

Basi bila kuangalia kwa makini, aliruka kwa pupa kuulekea mtungi huku akipiga kelele ya shangwe, pasi kujua kuwa ule ni mchoro tu. 

Matokeo yake akajibamiza kwenye bango na kujiumiza vibaya. 

Kwa kuwa alivunjika mbawa zake kwenye mshindo ule, alidondoka chini, na kukamatwa na jamaa mmoja mwenye uchu aliyekuwako kando.
Akafanywa kitoweo.
Share:

KISA CHA BWANA MWENYE WAKE WAWILI






 
Hapo zamani za kale, kulitokea bwana mmoja wa makamo ambaye alikuwa na wake wawili, mmoja mtu mzima na mwingine kijana; ambapo wote walimpenda sana, na kila mmoja alitamani awe anaendana naye. 

Na kwa wakati ule yule bwana nywele zake zilianza kuota mvi, jambo ambalo mke mdogo hakupendezwa  nalo, kwani lilimfanya aonekane ameolewa na mzee asiye makamo yake. 
Basi ikawa kila usiku alichukua chanuo akamchana nywele na kung'oa kila mvi anayofanikiwa kuiona. 

Lakini yule mke mkubwa alifurahi sana kuona mumewe anaota mvi, kwani hakupenda azeeke peke yake kwa maana angeweza hata kufananishwa na mama yake badala ya mke. Basi naye kila asubuhi alimkalisha mumewe na kuanza kumtengeneza nywele, huku akinyofoa nywele nyeusi kidogo kidogo zibaki mvi. 

Matokeo yake, muda si mrefu yule bwana akawa na kipara kabisaa, nywele zote kwisha!

ibot.isk@gmail.com
+255 757 242960  &  +255 655 242960
Share:

Kisa cha Simba Aliyezama Kwenye Mapenzi


Hapo zamani za kale,

Simba, mfalme wa mwitu, alitokea kumpenda binti mzuri wa jamaa mmoja mkata miti. Akapeleka maombi ya kinguvu ya kutaka amwoe. Baba wa binti yule, hakupenda kuruhusu mwanaye aposwe na mfalme Simba, lakini pia aliogopa kukataa ombi hilo. 

Akajikuta njiapanda, asijue akatae au akubali.
Hivyo ikamlazimu atumie mbinu kujinasua kwenye maswahibu hayo. 
Akamwambia mfalme Simba kwamba yeye yupo tayari kumwozesha binti yake, ila kwa sharti moja kuu: kwamba ataridhia ndoa hiyo iwapo ataruhusiwa kumng'oa Simba meno yake pamoja na kumkata makucha, akidai kuwa binti yake anaogopa sana vitu hivyo. 

Mfalme Simba kwa furaha akaafiki sharti hilo.

Basi ikawa siku aliporudi kwenda kuposa akiwa hana meno wala makucha, yule mkatamiti, akawa hamwogopi tena, akamtimua kwa marungu, na Simba akakimbia zake vichakani asirudi tena!
Share:

Alhamisi, 30 Januari 2014

HADITHI YA BIBI KIZEE NA CHUPA YA MVINYO

Bibi kizee aliokota chupa tupu ya mvinyo ambayo alitambua kuwa siku nyingi zilizopita ilijaa mvinyo. Ila alishangaa kuona kuwa hadi wakati huo ilikuwa ikitoa harufu mzuri ya kinywaji hicho.

Kwa uchu, aliisogeza chupa hiyo puani na kuvuta harufu yake, akaitazama, kisha akarudia kuinusa mara kadhaa na kusema kwa husuda,
Oo… kinywaji murua kabisa! Yamkini huu ulikuwa Mvinyo maridadi kwelikweli, kwa maana umeacha kwenye chupa hii harufu nzuri sana ya manukato!”

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

KISA CHA NG'OMBE NA CHURA

Ng’ombe Maksai alikwenda kunywa maji katika dimbwi ambalo lilikuwa na watoto wa chura. Watoto hao walizaliwa hapo na kwao hiyo ilikuwa ni maskani yao halali. Ila kwa wakati ule mama yao alikuwa ametoka, kaenda kuitembelea familia ya rafiki yake iliyokuwa na makazi kwenye dimbwi jingine upande wa pili wa kichaka.

Kwa bahati mbaya, Maksai alimkanyaga mtoto mmoja wa Chura na kumjeruhi vibaya, akafa. Punde mama yao akarejea toka matembezini na kubaini kuwa mmoja wa watoto wake hayupo dimbwini. Akawauliza wale nduguze kulikoni.

Mwenzetu amekufa, mama mpenzi;” alijibu mmoja wao kwa majonzi.
Kumetokea nini tena mbona niliwaacha wote wazima?” mama Chura alihoji.
Muda si mrefu uliopita mnyama mkubwa sana alikuja dimbwini akamkanyaga kwa kwato zake kubwa na kumuua.” walimjibu.

Chura alihamaki mno, akaanza kuvuta pumzi na kujitunisha kwa hasira, akahoji, “iwapo baradhuli huyo alikuwa mkubwa kiasi hicho kwa umbo,”
Ee mama yetu mpendwa, acha kujijaza upepo na kujitunisha” mtoto wake mmoja alimkatisha, “na wala usighadhibike kiasi hicho; kwani hakika nakuambia, utaanza kupasuka mwili kabla hujafanikiwa kuiga ukubwa wa dhalimu yule.”

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

Alhamisi, 2 Januari 2014

HADITHI YA MBWEHA NA CHUI

Siku moja mbweha na chui walizozana kuhusu nani kati yao alikuwa mzuri kuliko mwenzake. Chui alijinadi kwa kumwonyesha mbweha moja baada ya jingine madoa yaliyoipamba na kuipendezesha ngozi yake. Na kweli ukimwangalia Chui na madoa yake alionekana mzuri anayevutia.

Lakini mbweha naye alimkatiza kwa kusema, “hivi ni nani mzuri kati yako wewe, na mimi ambaye sijapambwa ngozi bali nimepambwa roho?”

Chui akaduwaa.

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

KISA CHA MWANADAMU NA SIMBA

Mwanadamu na Simba walikuwa wakisafiri pamoja kuelekea upande mwingine wa nchi. Wakiwa safarini walianza kutambiana, kila mmoja akijigamba kuwa ni mkuu na mwenye ushujaa na umahiri.

Wakati wakiendelea kubishana, walipita mahali ambapo kulikuwa na sanamu kubwa ya mawe ikimwonyesha “Simba akinyongwa na binadamu.” Msafiri yule alimwonyesha Simba sanamu ile na kusema kwa majivuno: “Unaona!... jinsi ambavyo binadamu tuna nguvu, na jinsi tunavyoweza kumshinda hata mfalme wa wanyama wote.”

Simba akamjibu: “Sikiliza rafiki yangu nikupashe, Sanamu hii tuionayo mbele yetu imechongwa na mmoja kati ya Binadamu. Laiti kama nasi Simba tungelikuwa na ujuzi wa kuchonga sanamu, ungeona sanamu ya Binadamu akiwa amefinywa chini ya kiganja cha Simba.”

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………
Share:

KISA CHA MCHEKESHAJI NA MWANAKIJIJI

Hapo zamani kulikuwepo mtu mmoja tajiri aliyeheshimika sana na watu wa jamii yake. Bwana huyo alifungua majumba ya maonyesho ya sanaa na watu wote waliruhusiwa kuingia bure. Wake kwa waume, watoto na wakubwa. Ikawa baada ya kazi nyingi za kutwa za kujitafutia riziki, Wananchi wakapata burudani na kufurahi pamoja.

Ila kwa kuwa maonyesho yalifanyika mara kwa mara, na wasanii walikuwa ni wale wale, na burudani ni zilezile zikijirudiarudia, siku zilipopita mambo yalianza kwenda doro kwa idadi ya wahudhuriaji kupungua na msisimko nao kushuka.

Yule tajiri alifikiri namna ya kufanya ili kuwarudisha watu katika uchangamfu kama awali.
Siku moja alitoa tangazo kwa umma akiahidi kutoa zawadi nono sana kwa mtu yeyote atakayeweza kufanya uvumbuzi wa aina mpya kabisa ya burudani jukwaani.
Watu kemkem wenye uzoefu katika tasnia ya kuburudisha umma kwa nyimbo, maigizo, vichekesho nk; walijitokeza kuishindania zawadi ile. 

Miongoni mwao alikuwapo Mchekeshaji ambaye alikuwa maarufu sana kutokana na vichekesho vyake mahiri.
Alijitokeza na kusema kuwa yeye ana aina mpya kabisa ya burudani ambayo haijawahi kuonyeshwa jukwaani kabla. Na wala hakuna mtu yeyote atakayeweza kushindana naye. Alijigamba, na walio wengi walimwamini.
Habari ile ilisambaa kama upepo na kuleta hamasa kubwa, ikawa gumzo kila pahali. Na siku ya shindano ilipofika ukumbi ulijaa ukatapika. Waliochelewa kufika walilazimika kusikiliza wakiwa nje.

Kila kitu kiliandaliwa vizuri na muda ulipofika mambo yakajiri kama ilivyopangwa.
Baada ya wengine kutoa burudani zao, kila mtu akishangiliwa na kutuzwa kwa kadiri yake, ikafika zamu ya yule aliyekuwa akisubiriwa kwa hamu.

Mchekeshaji alitokea jukwaani peke yake, bila kifaa cha aina yoyote wala washirika. Shauku kubwa ya matarajio chanya vilipelekea ukumbi kugubikwa na kimya kikuu. Watu wakisubiri kwa hamu kushuhudia kichekesho kipya walichoahidiwa na msanii yule nguli. Akiwa amevalia joho lake refu la rangi ya hudhurungi, ghafla alijipinda na kuinamisha kichwa chake kuelekea tumboni, kisha akatoa sauti kali ya kuiga mlio wa kitoto cha Nguruwe. Mlio huo aliouiga kwa sauti yake ulikuwa wa kupendeza kiasi kwamba hadhira ile ikamshuku kuwa huenda alikuwa ameficha kitoto cha Nguruwe kwenye vazi lake pana. Wakadai akaguliwe ili kuhakikisha, kabla hawajampa sifa na kumtawaza kuwa ni mshindi halali wa zawadi inayoshindaniwa.

Baada ya kufanya hivyo na kukutwa hana kitu chochote alichoficha, ukumbi ulilipuka kwa mayowe ya furaha na kushangilia usanii ule mpya.
Mwanakijiji mmoja miongoni mwa hadhira alipoyashuhudia yale yote, alipata wazo na kusema, “Nisaidieni enyi wakuu, mimi pia naweza, najua hawezi kunishinda katika kuiga sauti kama hii.” Na hapo hapo alitangaza kuwa ataigiza sauti kama vile siku inayofuata, na itakuwa kwa ubora na uhalisia zaidi. Na akawaomba wananchi watulie kwani mshindi wa kweli wa zawadi ile atatambulika baada ya yeye pia kupewa nafasi ya kusikilizwa.

Kesho yake umati mkubwa zaidi ulifurika kwenye jumba la maonyesho, wakiwa na mapenzi na ushabiki kwa Mchekeshaji, na wengi walikuja kwa lengo la kutaka kumdhihaki na kumsuta Mwanakijiji, na sio kushuhudia uwezo wake wa kuiga sauti vizuri kuzidi ile ya msanii aliyepita.
Wasanii wote walitokea jukwaani. Mchekeshaji alikuwa wa kwanza, alijiinamia tumboni na kuiga sauti ya kitoto cha nguruwe, kama siku iliyopita, na hadhira ilimshangilia sana kwa mbinja na vifijo.
Ndipo Mwanakijiji akapewa nafasi, akainama na kujifanya kama ameficha kitoto cha nguruwe kwenye vazi lake (ambapo ni kweli alikificha, ila hakuna aliyemshuku) alishika na kuyanyonga masikio, na mlio mkali wa kitoto cha nguruwe ulisikika.

Watazamaji, hata hivyo, walipaza sauti kwa pamoja wakisema kuwa yule Mchekeshaji aliyepita ndiye mshindi kwani aliiga mlio wa kitoto cha nguruwe kwa ufasaha zaidi. Wakataka Mwanakijiji aburuzwe nje ya jumba lile. Ndipo yule mshamba akakitoa kitoto halisi cha nguruwe kwenye mavazi yake, na kuionyesha hadhira ushahidi chanya kuhusu upotofu wa hukumu waliyotoa.

Tazameni,” alisema, “hii inadhihirisha wazi ninyi ni aina gani ya mahakimu!”

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

HADITHI YA TAI NA MBWEHA

Tai na Mbweha walikuwa marafiki wapenzi na hivyo walikubaliana kutoishi mbalimbali. Wakautafuta mti mmoja mzuri. Tai akajenga kiota chake kwenye matawi ya mti huo mkubwa, wakati Mbweha aliweka makazi yake kwenye shimo chini ya mti huo huo. Miezi michache baadaye Mbweha alizaa vitoto vinne.

Muda si mrefu baada ya makubaliano yao ya kuishi jirani kwa urafiki, Tai, kutokana na mahitaji yake ya chakula cha kuwalisha makinda wake, alishuka chini ya mti wakati rafiki yake Mbweha yupo matembezini, akakamata kitoto kimoja cha Mbweha, akakiua na kukila yeye na wanawe.

Mbweha aliporudi, aligundua kilichotokea, akahuzunika sana. Huzuni yake kuu haikuwa tu kwa kifo cha mtoto wake, bali pia ni jinsi ambavyo hakuwa na uwezo wa kulipiza kisasi kwa ukatili aliofanyiwa na rafiki yake, kwani asingeweza kupanda juu kwenye kiota cha Tai.

Hata hivyo muda si mrefu baadaye malipo ya udhalimu yalimfika Tai.
Akirukaruka kwenye mawindo sehemu fulani , ambako wanakijiji walikuwa wakitoa dhabihu ya mbuzi, ghafla akashuka na kudokoa pande la nyama, na kulichukua, pamoja na kizinga cha moto kilichoambatana nayo, bila kujua hadi kwenye kiota chake. Upepo mkali uliopovuma uliwasha moto kwenye kiota, hivyo wale makinda wake, kwa kuwa hawakuwa na mbawa bado, walishindwa kujiokoa wakaungua na kubanikwa kwenye kiota chao wakafa na kudondoka chini ya mti. 

Hapo chini, huku mama yao Tai akishuhudia, Mbweha akawala wote kwa kisasi.
Naye Tai alihuzunika sana.

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

KISA CHA MUUAJI

Mtu mmoja alimjeruhi mwenzie na kumuua. Ndugu na jamaa wa marehemu walianza kumkimbiza wakiwa na silaha kwa minajili la kumuua kwa kisasi.

Yule muuaji alikimbia kwa bidii kuu ili aokoe roho yake na hatimaye akafika kwenye kingo ya mto Nile. Ng’ambo ya mto alimwona Simba na kwa woga wake wa kuhofia kuuawa akaamua kukwea juu ya mti.

 Kule mtini pia aliona Joka kubwa kwenye matawi ya juu kwenye kilele, akaogopa sana kuuawa kwa sumu. Akaamua kujitupa mtoni ambako nako kulikuwa na Mamba. 

Alishikwa akauawa na kuliwa papo hapo.

Hivyo ardhi, anga na maji vyote kwa pamoja vilikataa kumficha Mwuaji yule.

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………
Share:

HADITHI YA SIMBA, MBWEHA NA WANYAMA WENGINE

Siku moja Simba alitangaza kuwa yu mgonjwa mahtuti na kwamba alikaribia kufa. Hivyo alitoa tamko la kuwaalika Wanyama wote waende nyumbani kwake kumwona na kusikia wosia wake wa mwisho na ushuhuda wa mambo kadha wa kadha, na pia wapate busara za mfalme.

Hivyo Mbuzi alienda kwenye pango alililoishi Mfalme Simba ili kumjulia hali. Alisimama kwenye sehemu ya kuingilia pangoni na kusikiliza kwa muda mrefu. Kisha kondoo alikuja na akaingia pangoni moja kwa moja, na kabla hajatoka Mwanafarasi naye alikuja kupokea wosia wa mwisho wa Mfalme, akaingia pangoni.

Baada ya muda mfupi Simba alijitokeza nje akionekana kupata nafuu ya haraka, akaja kwenye lango lake la kuingilia pangoni ili apunge upepo wa nje. Alipopiga macho kushoto na kulia alimwona Mbweha, akiwa amejiinamia anasubiri nje ya pango kwa muda mrefu.

Kwa nini ewe Mbweha hujaja ndani ya pango kutoa heshima zako za mwisho kwangu? Na badala yake unakaa tu hapa nje kwa kejeli?” Simba alimuuliza.

Nisamehe Bwana mkubwa,” Mbweha alijitetea, “ila katika kuja kwangu hapa nimegundua alama za nyayo za wanyama wengi ambao wamekwisha kukutembelea pangoni mwako; na nikichunguza kwa makini zaidi naona alama nyingi za kwato zikiingia ndani, na sioni zitokazo nje. Hadi hapo nitakapowaona wanyama waliokwishaingia pangoni mwako wakitoka nje, sitoingia, naona ni heri nibaki hukuhuku nje kwenye uwazi na hewa safi.”

Hadithi hii inatufundisha nini?
1……………………………………………………………………………………………………………………
2……………………………………………………………………………………………………………………
3……………………………………………………………………………………………………………………
Taja methali, nahau au msemo wa Kiswahili wenye maana inayofanana na maudhui ya hadithi hii;
………………………………………………………………………………………………………………………
………………………………………………………………………………………………………………………

Share:

Live Traffic Feed

Blogroll

BTemplates.com

Inaendeshwa na Blogger.

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Popular Posts

Kumbukumbu la Blogu