Hadithi za kale zenye mafundisho za Esopo zilizoandikwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Zimetafsiriwa kwa Kiswahili na Issa S. Kanguni, chini ya shirika lisilo la kiserikali la Tanzania Inventors and Techno-Thinkers Consortium (TITC). Tel; +255757242960

Tafuta katika Blogu Hii

Pages

Ijumaa, 30 Mei 2014

KISA CHA PANYA WA MJINI NA PANYA PORI

Panya Pori alimwalika panya wa mjini, ambaye ni rafiki yake kipenzi, amtembelee kwake aje ajionee maisha ya porini. Wakiwa kwenye uwanda wazi wa mashamba, wakila mabaki ya nafaka na mizizi ya miti iliyong’oka, Panya wa Mjini alimwambia rafiki yake, 
 “Huku shamba rafiki yangu unaishi maisha ya wadudu, yaani kama mchwa ama sisimizi, wakati mimi kule nyumbani kwangu ni neema tupu ya vyakula kedekede.  Yaani nimezungukwa na kila aina ya raha na anasa, na iwapo utakubali kufuatana nami nyumbani, kama ninavyoamini utakubali, nawe utapata kufaidi sehemu ya mapochopocho yangu.” 

Kwa maneno yale, Panya Pori akashawishika kiurahisi, na akakubali kuandamana na rafiki yake katika safari ya kurudi mjini. Walipofika, Panya wa Mjini akamtengea rafikiye mlo wa mkate, shayiri, maharagwe, matini yaliyokaushwa, asali, zabibu kavu, na, mwishowe, alimletea kipande kinono cha jibini toka kapuni. Panya Pori, akiwa na furaha isiyo kifani kwa kupata chakula kizuri na kingi kama kile, alishukuru kwa unyenyekevu na kuyalaani maisha yake magumu kule shamba. 

Basi wakiwa ndo wanataka kuanza kula, bwana mmoja akafungua mlango, na wote wawili wakatimka mbio kadri ya uwezo wao na kuingia kwenye kijishimo chembamba kilichowatosha kwa kujibana. Baadaye wakatoka, na kwa mara nyingine kabla hata hawajaanza kula, mtu mwingine akafungua mlango na kuingia kuchukua kitu fulani kabatini, ambapo wale panya wawili, wakiwa na hofu zaidi ya mara ya kwanza, walikimbia na kwenda kujificha tena. 

Mwishowe yule Panya Pori, huku akitweta na akiwa ameshikwa na njaa kwelikweli, akamwambia rafiki yake: 
“Japokuwa umeniandalia mlo maridhawa, sina budi kuondoka na kukuachia uufaidi mwenyewe. Chakula chako kimezungukwa na hatari nyingi mno, siwezi kukifurahia hata kidogo.  Kwangu mimi ni heri maisha ya  kuokoteza nafaka na kuguguna mizizi porini, ambako ninaishi kwa usalama, bila hofu yoyote.”
Akaenda zake.
***
Share:

0 maoni:

Chapisha Maoni

Live Traffic Feed

Blogroll

BTemplates.com

Inaendeshwa na Blogger.

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Popular Posts

Kumbukumbu la Blogu