Hadithi za kale zenye mafundisho za Esopo zilizoandikwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Zimetafsiriwa kwa Kiswahili na Issa S. Kanguni, chini ya shirika lisilo la kiserikali la Tanzania Inventors and Techno-Thinkers Consortium (TITC). Tel; +255757242960

Tafuta katika Blogu Hii

Pages

Jumamosi, 31 Mei 2014

KISA CHA NYIGU NA NYOKA

Nyigu alitua kwenye kichwa cha Nyoka na kuanza kumng’ata mfululizo, akimjeruhi vibaya kwa lengo la kutaka kumwua. 
Nyoka, akiwa katika maumivu makali asijue namna ya kujiokoa na adui yake huyo, mara akaona mkokoteni uliojazwa magogo ya miti ukipita. 

Basi kwa makusudi akaamua kwenda njiani na kuweka kichwa chake chini ya gurudumu, akasema, 
“Angalau, mimi na adui yangu tuangamie sote pamoja.”
***

1. Hadithi hii inatufundisha nini?
2. Taja methali au nahau ya kiswahili yenye maana sawa na maudhui ya hadithi hii.
Share:

KISA CHA MITUNGI MIWILI

Mitungi miwili iliachwa kwenye ukingo wa mto, mmoja wa chuma, na mwingine wa udongo. 
Baada ya mvua kubwa kunyesha mbali mto utokako ndipo maji ya mto yalipoongezeka na hatimaye mitungi yote ilisombwa ikaelea kufuata mkondo. 

Basi ule mtungi wa udongo ukawa unafanya jitihada kwelikweli kujiweka mbali na ule wa chuma. Kuona vile, Mtungi wa chuma ukatabasamu na kuuambia ule wa udongo: 
“Usihofu rafiki yangu, mi sikugongi.”


“Sawa, lakini inawezekana nikagusana nawe,” ukasema mtungi wa udongo, “iwapo nitakukaribia; kwani haijalishi wewe ukinigonga, au mimi nikakugonga, nitadhurika tu.”
***
Share:

Ijumaa, 30 Mei 2014

KISA CHA MAADUI WAWILI

Jamaa wawili, ambao walikuwa ni maadui wa kufa na kupona, walijikuta wakisafiri katika merikebu moja. Wakiwa wamepania kukaa mbalimbali kadri iwezekanavyo, mmoja alienda kukaa nyuma kabisa na  mwingine mbele kabisa kwenye ncha ya mwisho ya merikebu. 

Mara kukapiga dhoruba kali na mawimbi yakaanza kukipeleka chombo mrama, na kilipokuwa kwenye hatari ya kuzama, yule jamaa aliyekaa nyuma akamuuliza nahodha ni upande upi wa merikebu ile ungelianza kuzama kabla ya  mwingine. 
Alipomjibu kwamba anaamini ni upande wa mbele utakaozama kwanza, yule jamaa akasema, 
“Kifo hiki hakitokuwa na mateso kwangu, endapo tu nitafanikiwa kumwona yule rafiki yangu pale akitapatapa na kufa kabla yangu.”
***
Share:

KISA CHA PANYA WA MJINI NA PANYA PORI

Panya Pori alimwalika panya wa mjini, ambaye ni rafiki yake kipenzi, amtembelee kwake aje ajionee maisha ya porini. Wakiwa kwenye uwanda wazi wa mashamba, wakila mabaki ya nafaka na mizizi ya miti iliyong’oka, Panya wa Mjini alimwambia rafiki yake, 
 “Huku shamba rafiki yangu unaishi maisha ya wadudu, yaani kama mchwa ama sisimizi, wakati mimi kule nyumbani kwangu ni neema tupu ya vyakula kedekede.  Yaani nimezungukwa na kila aina ya raha na anasa, na iwapo utakubali kufuatana nami nyumbani, kama ninavyoamini utakubali, nawe utapata kufaidi sehemu ya mapochopocho yangu.” 

Kwa maneno yale, Panya Pori akashawishika kiurahisi, na akakubali kuandamana na rafiki yake katika safari ya kurudi mjini. Walipofika, Panya wa Mjini akamtengea rafikiye mlo wa mkate, shayiri, maharagwe, matini yaliyokaushwa, asali, zabibu kavu, na, mwishowe, alimletea kipande kinono cha jibini toka kapuni. Panya Pori, akiwa na furaha isiyo kifani kwa kupata chakula kizuri na kingi kama kile, alishukuru kwa unyenyekevu na kuyalaani maisha yake magumu kule shamba. 

Basi wakiwa ndo wanataka kuanza kula, bwana mmoja akafungua mlango, na wote wawili wakatimka mbio kadri ya uwezo wao na kuingia kwenye kijishimo chembamba kilichowatosha kwa kujibana. Baadaye wakatoka, na kwa mara nyingine kabla hata hawajaanza kula, mtu mwingine akafungua mlango na kuingia kuchukua kitu fulani kabatini, ambapo wale panya wawili, wakiwa na hofu zaidi ya mara ya kwanza, walikimbia na kwenda kujificha tena. 

Mwishowe yule Panya Pori, huku akitweta na akiwa ameshikwa na njaa kwelikweli, akamwambia rafiki yake: 
“Japokuwa umeniandalia mlo maridhawa, sina budi kuondoka na kukuachia uufaidi mwenyewe. Chakula chako kimezungukwa na hatari nyingi mno, siwezi kukifurahia hata kidogo.  Kwangu mimi ni heri maisha ya  kuokoteza nafaka na kuguguna mizizi porini, ambako ninaishi kwa usalama, bila hofu yoyote.”
Akaenda zake.
***
Share:

KISA CHA MBWA WAWILI

Kulitokea bwana mmoja ambaye alifuga mbwa wawili: 
Mbwa mwindaji, ambaye alimfundisha kumsaidia katika kazi zake za uwindaji, na Mbwa mlinzi, aliyemfundisha kulinda nyumba. 

Kila aliporejea nyumbani kutoka mawindoni, alikuwa akimpa yule Mbwa wa nyumbani minofu mikubwa mikubwa ale. Mbwa mwindaji hakupendezwa na jambo lile na alishindwa kuvumilia, alimfuata mwenzie, akamwambia, 

“Ni mateso makubwa kufanya kazi ngumu kama nifanyayo mimi, ilhali wewe, ambaye husaidii lolote katika kuwinda, unajibarizi na kufaidi matunda ya jasho langu.” 

Mbwa wa nyumbani akamjibu, 
“Rafiki yangu, usinilaumu mimi bali umlaumu bwana wetu, ambaye hajanifundisha mimi kufanya kazi bali kuishi kwa kutegemea matunda ya kazi za wengine.”
***
Share:

Alhamisi, 22 Mei 2014

Kisa cha Bwana Mzalendo mwenye Kipawa

Baada ya kufanikiwa kupewa nafasi ya kusikilizwa na mfalme na baraza lake la washauri, Mzalendo mwenye kipaji alitoa karatasi mfukoni mwake, akasema: 
Share:

Jumapili, 18 Mei 2014

KISA CHA TAI, PAKA NA NGURUWE PORI

Kulitokea Tai mmoja ambaye alijenga kiota chake juu ya mti mkubwa; Paka naye, baada ya kuona kuna shimo linalomfaa, alihamia na kuanza kuishi katikati ya shina la mti ule ule; na Nguruwe pia, akiwa na vitoto vyake, akaweka makazi kwenye shimo lililopo wazi chini ya mti ule. 

Basi ikawa Paka, kwa tabia yake mbaya, akaanza kutengeneza hila ili kuvuruga kusanyiko lile la kudra la familia tatu tofauti katika mti mmoja. Ili kutekeleza njama yake, alianza kwa kupanda juu kwenye kiota cha Tai, akamwambia, 
"Ndugu yangu, angamizo linakaribia kushuka juu yako, na mimi pia, kwa bahati mbaya. Jirani yetu Nguruwe-pori, ambaye unamwona kila siku akichimbua chimbua ardhi kwa mdomo wake, anataka kuung'oa mti huu, ili utakapoanguka akamate familia yako na yangu kwa ajili ya chakula kwa watoto wake." 

Baada ya kufanikiwa kumwogofya Tai kiasi kile, Paka alishuka chini kabisa na kwenda kwenye shimo la Nguruwe-pori, akamwambia, "Ndugu yangu, maisha ya watoto wako yapo hatarini; kwani punde tu utakapothubutu kutoka kwenda kutafuta chakula, Tai amejiandaa kushambulia mmoja wa watoto wako, kwa ajili ya chakula cha familia yake." 
Alipofanikiwa kumjaza hofu Nguruwe-pori, Paka akaenda zake kwake na kujifanya kana kwamba naye anajificha kwa woga kwenye shimo lake. Ilipofika nyakati za usiku kila siku alinyata na kutoka kinyemela kwenda kutafuta chakula kwa ajili yake na wanawe, huku akijifanya kuogopa na kuwalinda wanawe mchana kutwa.

Wakati huo, Tai,  akiwa ana hofu kuu dhidi ya Nguruwe-pori, alikaa kwenye kiota chake kutwa kucha, ilhali Nguruwe pori naye, akiwa na hofu kuu dhidi ya Tai, hakuthubutu kutoka kwenye shimo lake. 
Kwa hali hiyo, wote pamoja na familia zao, waliangamia kwa njaa, na kumwacha Paka na wanawe wakijivinjari kwa nafasi.
***
Share:

KISA CHA MARAFIKI WAWILI NA DUBU

Marafiki wawili walikuwa wakisafiri pamoja kupitia vichakani, mara akatokea dubu mkubwa na kuanza kuwakimbiza.
Katika harakati za kutaka kujiokoa walikimbia na ikawa mmoja kati yao alikuwa mbele na mwingine nyuma yake. 

Basi yule wa mbele iliwahi kulishika tawi la mti na kujificha peke yeke kwenye majani. Mwenzake, kwa kuona amechelewa na hana namna, alijitupa chini na kulala kifudifudi, huku akijilegeza kama mfu. Dubu alipomfikia, aliweka pua yake sikioni kwa yule bwana, akanusa na kunusa. 

Mwishowe, Dubu akaguna kwa nguvu huku akijitikisa kichwa na kuenenda zake, kwani Dubu huwa hawali mizoga. 

Ndipo yule bwana aliyejificha peke yake kwenye mti akaja kumfuata rafiki yake, na, huku akicheka, akasema "Kakunong'oneza nini yule bwana mkubwa?" 
"Ameniambia kwamba," alijibu yule bwana, "Kamwe usimwamini rafiki anayekutelekeza wakati wa shida."
***
Share:

Jumamosi, 17 Mei 2014

KISA CHA BAHILI NA DHAHABU ZAKE

Bwana mmoja bahili aliuza vitu vyake vyote alivyonavyo na kununua sarafu za dhahabu, ambazo alichimba shimo na kuzifukia chini kando ya ukuta wa zamani na kuwa anakwenda kuziangalia kila siku. Mmoja wa wafanyakazi wake aligundua safari zake za mara kwa mara kwenda eneo lile na akaanza kumchunguza zaidi. 

Muda mfupi tu baadaye aling'amua siri ya ile hazina iliyofichwa, na alipochimbua na kukuta rundo la dhahabu, akaziiba. Yule bwana bahili, alipofika siku iliyofuata, alikuta shimo tupu na akaanza kulia na kuvuta nywele zake hata kuzinyofoa kwa hasira na majonzi. Jirani yake, baada ya kumwona akiwa katika hali ile ya huzuni kupita kiasi, na alipogundua sababu ya huzuni ile, alimwambia 
"Ndugu, hakuna haja ya kuhuzunika kiasi hicho; bali nenda na uchukue jiwe, liweke humo shimoni na ufunike, kishakila siku kuangalia na jifanye kana kwamba dhahabu zako bado zimo humo. Itakufaa kwa hali ile ile; kwani hata kabla ya kuibiwa haukuwa nayo dhahabu, kwa kuwa uliifukia tu na hukuitumia kwa namna yoyote ile."
***
Share:

KISA CHA MBWA NA MBWA MWITU

Mbwa-mwitu mmoja dhaifu alikuwa akikaribia kufa kwa njaa na mara kwa bahati akakutana na mbwa wa nyumbani ambaye alikuwa akipita. 
"Ah, binamu," alisema mbwa "nilijua tu yatakukuta haya; kwamba maisha yako ya kutangatanga na yasiyo na uhakika ipo siku yatakuangamiza. Kwanini usifanye kazi maalum na ya uhakika kama nifanyavyo mimi, ili upate chakula kila mara kama nipatavyo  mimi?" 
"Nakubaliana na wewe kabisa ndugu yangu," alijibu Mbwa-mwitu, "endapo tu nikipata nafasi." 
"Nafasi sio tatizo, mi ntakufanyia mpango," alisema Mbwa; "twende nami nyumbani kwa bwana wangu na nitamwomba akuajiri tufanye kazi pamoja nami." 

Basi Mbwa-mwitu na Mbwa wakaongozana kuelekea mjini. Wakiwa bado njiani, wanakaribia kufika Mbwa-mwitu akagundua kwamba nywele kwenye sehemu fulani ya shingoni ya Mbwa zimenyonyoka na kubaki chache, hivyo akamuuliza Mbwa kulikoni. 
"Oh, wala si kitu," Mbwa alijibu. "Hii ni sehemu ambayo mkanda wa nyororo hufungwa nyakati za usiku ili kunifanya nibaki sehemu moja; unauma na kukera kidogo, ila baada ya muda unazoea." 

"Ha ndiyo hivyo?" alisema mbwa mwitu. "Basi kwaheri ndugu yangu, Bwana Mbwa."
***
Share:

KISA CHA MBWA NA SUNGURA

Mbwa mwindaji alimvumbua Sungura kwenye mafukutu juu ya kilima na kuanza kumkimbiza kwa kitambo, wakati fulani alimkaribia na kung'ata kwa nguvu kwa meno yake makali kana kwamba ataka kumuua, na mara nyingine alimkumbatia kana kwamba anacheza na mbwa mwenzake.

 Yule Sungura akamwambia, "natamani ungekuwa mkweli kwangu, na kuonyesha dhamira yako halisi. Kama we ni rafiki, kwa nini umening'ata kiasi hiki? na kama we ni adui, kwa nini basi unacheza nami?"
***
Share:

KISA CHA MZEE KIPARA NA MBUNG'O

Mbung'o alitua kichwani kwa Mzee mmoja na kumng'ata kwenye sehemu yenye kipara, ambapo yule Mzee kwa kutaka kumwangamiza Mbung'o alijipiga kofi pwaaa! 

Yule mbung'o alifanikiwa kukwepa na aliondoka akisema kwa dhihaka, 
"Ulipanga kulipiza kisasa, hata kwa kuua, maumivu madogo tu ya kung'atwa na mdudu kama mimi, ona sasa ulivyojitenda na kujiongezea maumivu juu ya maumivu?"

 Mzee kipara akamjibu, 
"Ni rahisi kwangu kujisamehe maumivu ninayojipa mwenyewe, kwani najua hakukuwa na nia ya kujiumiza. Lakini wewe, mdudu baradhuli mwenye tabia ya kunyonya damu za watu, natamani ningelifanikiwa kukuua hata kama ningalipata maumivu makubwa zaidi ya haya niliyopata sasa."
***

Share:

KISA CHA MAMA NA MTETEA

Hapo zamani za kale kulikuwako mama mmoja ambaye alikuwa na kuku wake mtetea aliyetaga yai moja kila siku.

 Kila wakati yule mama alifikiri na kujiuliza atawezaje kupata mayai mawili kwa siku badala ya moja, na mwishowe, ili kutimiza azma yake, akaamua kuanza kumlisha yule kuku mara mbili ya shayiri za chakula alichokuwa akimpa kwa siku.

Basi kuanzia siku hiyo yule kuku alinenepa
sana na kuwa mtepetevu, na hakutaga tena.
***

Share:

KISA CHA MBWEHA ALIYEKATWA MKIA

Hapo zamaini za kale, kulitokea Mbweha mmoja mjanja. Siku moja kwenye pitapita zake kwa bahati mbaya alinaswa mtegoni, na katika kuhangaika alifanikiwa kujinasua, ila alikatika mkia ukabakia kipisi kifupi tu.

Siku za mwanzo mwanzo aliona aibu kujionyesha ulemavu wake wa kutokuwa na mkia kwa mbweha wenzake. Baadaye akaamua kujibaraguza na kufanya kana kwamba kukosa mkia si kitu, akawaalika Mbweha wote kwenye mkutano mkuu, ili wajadili pendekezo alilo nalo moyoni.

Walipokusanyika, Mbweha alitangaza pendekezo lake, kwamba eti mbweha wote ni vyema wakakata mikia yao na kubaki na vipisi kama yeye.  Akasema kwamba mkia ni mzigo wanapokuwa wanafukuzwa na maadui zao, mbwa; na pia unasumbua wanapohitaji kuketi kitako wazungumze mambo kirafiki na wenzi wao. Akapaza sauti na kudai kuwa haoni faida yoyote ya wao kuendelea kubeba zigo la mkia usio na tija yoyote.

“Hiyo ni sawa kabisa,” akajibu mbweha mmoja mzee; “ila sidhani kama ungelitoa pendekezo la kukata mikia ambayo ni kifaa chetu muhimu, laiti kama wewe mwenyewe usingalipatwa janga la kupoteza mkia wako.”
***
Share:

Jumatano, 7 Mei 2014

KISA CHA MBWEHA, MBWA MWITU NA NYANI

Mbwa mwitu alimshutumu  vikali Mbweha kwa kumwibia, ila Mbweha alikana katukatu kwamba hakutenda kosa hilo. Baada ya kuzozana kwa muda, wakampelekea Nyani shauri hilo ili atoe hukumu na kumaliza mgogoro baina yao. 

Basi baada ya kila mmoja wao kupewa nafasi ya kujieleza kwa kina, Nyani akatangaza hukumu ifuatayo: 
"Siamini katu kwamba wewe, Mbwa mwitu, umepotelewa na hicho unachodai kuibiwa; na ninaamini kabisa kwamba wewe, Mbweha, umeiba hicho unachokataa katakata kuwa hujaiba."
***

Hadithi hii inatufundisha nini? Jibu ujishindie.
Share:

KISA CHA WASAFIRI WAWILI NA SHOKA

Jamaa wawili walikuwa wakisafiri pamoja. Wakiwa njiani mmoja wao aliokota shoka zuri lililokuwa limelazwa kando ya njia, akalichukua na kusema, 

"Nimeokota shoka." 
"Hapana rafiki yangu," mwenzake alimjibu, "usiseme 'Nimeokota' bali 'Tumeokota' shoka." 

Basi kabla hata hawajafika mbali wakamwona mwenye shoka lake akiwafuata kwa hasira, ndipo yule aliyeliokota shoka akasema, "Duh! tumekwisha." 

"La hasha," alijibu yule mwenzake, "endelea na ile kauli yako ya awali, rafiki yangu; kile ulichoona sahihi wakati ule, kione kuwa sahihi hata sasa. Sema 'Nimekwisha', sio 'Tumekwisha'."
***
Share:

Live Traffic Feed

Blogroll

BTemplates.com

Inaendeshwa na Blogger.

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Popular Posts

Kumbukumbu la Blogu